1


                                QUITO, ECUADOR
KUNA Lionel Messi mmoja tu duniani. Huyu hapa wa Jumatano usiku pale Ecuador. Amefanya maajabu ambayo dunia ilikuwa inamtarajia ayafanye na kweli akayafanya. Amepiga ‘hat trick’ ambayo imeipeleka Argentina katika fainali za Kombe la Dunia mwakani.
Argentina ilikuwa inakaribia kuzikosa fainali hizo na ilihitaji kushinda mchezo huo wa ugenini Ecuador katika Jiji la Quito ambalo lipo futi 9350 kutoka usawa wa habari huku kukiwa na hali ya hewa nzito. Messi akasahau yote hayo na kuibuka shujaa wa Wargentina.
Ushindi huo wa mabao 3-1 sasa umeipeleka Argentina mpaka nafasi ya tatu katika kundi lao la Amerika Kusini na kuungana na Brazil, Uruguay na Colombia kufuzu moja kwa moja katika fainali hizo zitakazofanyika Russia Juni mwakani huku Peru ikisubiri kucheza pambano la mtoano na New Zealand.
Hata hivyo, mambo yalianza kuwa mabaya kwa Argentina katika sekunde 40 tu za pambano hilo baada ya kutanguliwa kwa bao la Ecuador lililofungwa na Renato Ibarra. Kuanzia hapo Messi alionyesha kiwango bora zaidi kwa mchezaji binafsi katika jezi ya Argentina.
Alifunga bao la kusawazisha katika dakika 12 kabla hajaongeza jingine dakika nane baadaye katika dakika ya 20. Kipindi cha pili, Messi aliufunga mchezo kwa kupiga hat trick katika dakika ya 62 na hivyo kuinyamazisha dunia ambayo ilikuwa na wasiwasi huenda Argentina isifuzu Kombe la Dunia.
Hiyo ilikuwa hat trick yake ya 44 katika maisha yake ya soka na pia amerudisha uwezekano wa kutwaa taji la Kombe la Dunia, kitu ambacho amekuwa akikisubiri kwa hamu katika maisha yake yote ya soka tangu awe staa.
Kocha wa Argentina, Jorge Sampaoli mara baada ya pambano hilo alidai Messi ndiye mchezaji bora zaidi duniani kwa sasa huku Messi alikuwa hadaiwi Kombe la Dunia na Argentina, bali Kombe la Dunia lilikuwa linamdai Messi.
“Leo kwa bahati tu utaifa wa mchezaji bora zaidi duniani ni wa Muargentina. Lazima tuhakikishe sio kila kitu kinamtegemea Messi lakini leo ameonyesha uwezo wake. Niliwaambia wachezaji, ‘Messi alikuwa hadaiwi Kombe la Dunia na Argentina, bali Kombe la Dunia lilikuwa linamdai Messi’ Tumsaidie afike katika Kombe la Dunia,” alisema Sampaoli.
“Nadhani mechi ilianza kutuchanganya kwa maana ya mipango yetu ilikuwa migumu zaidi kwa sababu Ecuador ilifunga bao katika dakika ya kwanza. Hata hivyo, sisi kama kundi tuliamini mechi inaisha katika dakika 90,” alisema Sampaoli.

Na sasa Messi anakwenda katika fainali za Kombe la Dunia sambamba na staa mwenzake katika soka la kileo, Cristiano Ronaldo ambaye aliiongoza Ureno kuichapa Uswisi katika mchezo muhimu wa Ureno na hivyo kujihakikishia safari ya Russia. Hata hivyo, Ureno haikuwa katika tishio kubwa kama Argentina.

Mastaa wakubwa ambao wataikosa safari ya Russia ni pamoja na nyota wawili wa Chile, Alexis Sanchez na Arturo Vidal ambao katika mchezo wa mwisho dhidi ya Brazil juzi usiku walichapwa mabao 3-0 na Brazil katika Jiji la Sao Paulo, Brazil.
Staa mwingine ambaye atazikosa fainali hizo ni nyota wa kimataifa wa Wales, Gareth Bale ambaye kikosi chake cha Wales licha ya kuonyesha mambo makubwa katika Euro 2016 iliyofanyika Ufaransa lakini kimeshindwa kuonyesha makali yake katika mechi za kufuzu.
Mastaa wengine wakubwa ambao watakuwepo katika fainali zijazo za Kombe la Dunia ni pamoja na Neymar, Kylian Mbappe, Antoine Griezmann, Luis Suarez, Paul Pogba, Eden Hazard, Alexandre Lacazette na wengineo.

Post a Comment

  1. 2017 ford fusion hybrid titanium - TiG
    Discover titanium or ceramic flat iron premium and titanium exhaust premium titanium watches at a boutique boutique brand. Get grade 23 titanium the best 4x8 sheet metal prices near me deals titanium build and offers of TiG in an instant.

    ReplyDelete

 
Top