AMSTERDAM,
UHOLANZI
SERGIO KUN AGUERO
amepata ajali mbaya ya gari akiwa Uholanzi na atalikosa pambano la Jumamosi huku
akitarajiwa kukosa mechi nyingine kadhaa.
Aguero
alikuwa abiria katika teksi iliyopata ajali wakati akitoka katika tamasha
kubwa la mwanamuziki maarufu wa Colombia, Maluma Alhamisi usiku huku akielekea
uwanja wa ndege kwa ajili ya kurudi England kujiandaa na pambano dhidi ya Chelsea.
Hata
hivyo, dereva wa teksi hiyo alipoteza mwelekeo na gari hilo likagonga nguzo za
kando ya barabara na ingawa staa huyo wa kimataifa wa Argentina alikuwa
amefunga mkanda lakini bado alivunjika baadhi ya mbavu zake.
Habari
zaidi zinadai kuwa, Aguero anaweza kuwa nje kwa wiki sita hadi nane kutokana na
majeraha hayo huku pia akitazamiwa kukosa mechi mbili muhimu za Argentina za
kufuzu michuano ya Kombe la Dunia dhidi ya Peru itakayochezwa Oktoba 5 na ile
dhidi ya Ecuador itakayochezwa Oktoba 10.
Klabu
yake ya zamani ya Independiente ya Argentina ambayo ilimuuza Aguero kwenda
Atletico Madrid Mei 2006 kwa dau la Euro 23 milioni ilikuwa ya kwanza kumtakia
afya njema staa wao huyo wa zamani wakiandika: “Tunakutakia nguvu na upone
haraka. Independiente yote ipo na wewe katika wakati huu mgumu.”
Aguero
pia amekuwa akitoka kimapenzi na mwanamuziki maarufu wa Argentina, Karina
Tejeda ambaye alikutana naye baada ya kuachana na mtoto wa staa wa zamani wa
soka wa Argentina, Diego Maradona, Gianina Maradona ambaye amezaa naye mtoto
mmoja, Benjamin Aguero.
Hilo
ni pigo la pili kwa Kocha wa Manchester City, Pep Guardiola ambaye juzi
ilithibitika kuwa huenda akamkosa beki wake wa kushoto, Benjamin Mendy kwa
msimu mzima baada ya kuumia vibaya goti lake katika pambano dhidi ya Crystal
Palace wikiendi iliyopita.
Timu
ya madaktari wa Manchester City ilikuwa ina matumaini kwamba huenda staa huyo
wa kimataifa wa Ufaransa alikuwa ameumia kidogo na angeweza kwenda Barcelona kwa
ajili ya kukutana na mtaalamu wa goti, Dr Ramon Cugat.
Hata
hivyo, vipimo vimeonyesha aliumia vibaya sehemu ya ndani ya goti na Alhamisi
alitazamiwa kufanyiwa upasuaji na ingawa City haijasema atakuwa nje kwa muda
gani lakini kwa aina ya majeraha yake anatazamiwa kuwa nje hadi miezi tisa.
Mendy
alidhani angerudi uwanjani mapema baada ya kuandika katika mtandao wake wa
Twitter akisema :“Habari mbaya jamani. Nitajiunga kwa mkopo katika klabu ya majeruhi
kwa miezi kadhaa lakini natazamiwa kurudi haraka nikiwa imara.”
Kocha
wa City, Pep Guardiola alisema mara baada ya pambano la Jumanne dhidi ya
Shakhtar Donetsk ambalo walishinda akiweka wazi hofu yake kwamba Mendy alikuwa
ameumia zaidi kuliko alivyofikiria awali.
Kuumia
kwa Mendy kunamuacha Guardiola akiwa na beki halisi wa upande wa kushoto huku
akitoa ishara huenda akaingia sokoni kwa ajili ya kununua beki mwingine wa
upande wa kushoto.
Post a Comment