LONDON, ENGLAND
ANTONIO CONTE (pichani chini) ameyadharau
madai yaliyotolewa na straika wake, Diego Costa kufuatia mahojiano ya hivi
karibuni akidai Chelsea inamtendea kama mhalifu.
Na kocha huyo wa Chelsea
ameweka wazi msimamo wake kuwa straika huyo hakutakiwa kurudi katika mipango
yake na kusisitiza mambo ya Costa yameshapita, pamoja na klabu kumtaka nyota
huyo wa kimataifa wa Hispania kurudi Magharibi mwa London.
Conte alikumbana na
swali hilo kwa mara ya kwanza tangu Costa alipofanya mahojiano, na kumtuhumu
kocha huyo Muitaliano kumtendea kama mtuhumiwa na kudai hatarudi Chelsea hata
kama klabu hiyo itendelea kumpiga faini.
Pia, Costa
aliendeleza vita yake ya maneno na Chelsea na Conte kwa kudai mabingwa hao wa
Ligi Kuu wanataka kumuuza bei ya ghali na kuzima ndoto zake za kurudi Atletico
Madrid.
Chelsea inataka
kumuuza Costa kwa Pauni 50 milioni, Atletico Madrid iko tayari kulipa Pauni 30
milioni. Chelsea ilimnunua staa huyo kutoka
Atletico Madrid mwaka 2014 kwa Pauni 32 milioni.
“Ninachofahamu Chelsea
inataka ofa kubwa kuliko ile iliyolipa kwa ajili yangu. Wakala wangu alisema Chelsea
inataka pesa ambayo Atletico haitaweza kuikaribia. Lakini kama Atletico na Chelsea
hazitafikia makubaliano na Atletico haitaonyesha jitihada, sitataka kuitumikia
klabu ambayo haitaonyesha jitihada na kunisajili.
“Pindi niliposikia
kuwa, Conte hanitaki, wakala wangu alizungumza na Atletico kama itataka nirudi.
“Bila shaka kwa moyo
mkunjufu na heshima niliyoipata pale, walionyesha kuvutiwa. Lakini hawakulipa
pesa. Atletico ni timu inayokua kila mwaka, ni timu kubwa lakini haiwezi kulipa
kiasi kikubwa zaidi.
Costa akiwa nyumbani kwao, Brazil
"Chelsea ilipanga
kuniuza katika klabu kadhaa, lakini nilikuwa muwazi kwao, Nilisema kama sipo
katika mipango ya kocha, ninataka kuchagua sehemu ya kwenda. Sitawaachia wao
waamue kwa kutaka pesa nyingi.’
Alipoulizwa
alichokisema Costa, Conte alicheka kabla ya kujibu: “Ni vizuri, ninapenda
kucheka.
“Ninaweza kuwaambia kila
mmoja aliyekuwa ndani ya Chelsea anafahamu nini kilitokea msimu uliopita kwa Diego.
Sipendi kuendeleza hii kitu. Kwangu, imeshapita.”
Chama cha Wachezaji
wa Kulipwa (PFA) kinaweza kutoa suluhisho la dharula kutokana na kuongezeka kwa
mgogoro huu.
Kwa mtazamo wa Costa utahitajika
usuluhishi wa PFA lakini chama hicho huwa kinawasaidia wachezaji ambao wako
ndani ya klabu.
PFA iliwahi kuhusika
kutatua mgogoro wa Luis Suarez na Liverpool miaka mitatu iliyopita wakati
alipokatazwa kufanya mazungumzo na Arsenal.
Post a Comment