MANCHESTER, ENGLAND
KOCHA Louis van Gaal amekiri kufanya makosa
makubwa kwa kuwaondoa washambuliaji wake akiwemo Javier Hernandez ‘Chicharito’
katika kikosi cha Manchester United wakati wa dirisha lililopita la usajili.
Mdachi huyo aliwafungulia milango wa kutokea
washambuliaji watano, akiwamo fowadi huyo wa Mexico, ambaye amekuwa moto kweli
tangu alipotua kwenye Bundesliga na kwamba anamuumbua.
Chicharito ambaye jina lake jingine la utani ni
Little Pea alijiunga na Bayer Leverkusen kwa ada ya Pauni 7.3 milioni.
Mshambuliaji huyo amefunga mabao 19 katika mechi
22, ikiwa ni mabao mengi kuliko waliofunga washambuliaji wote wa Man United, Wayne
Rooney, Anthony Martial na Memphis Depay kwa msimu huu.
Mbaya zaidi, Chicharito ambaye alisema aliambiwa
na Van Gaal kwamba ana asilimia moja tu ya kupata namba kama atabaki Old
Trafford, amechaguliwa kuwa mchezaji bora wa mwezi kwenye Bundesliga kwa mara
ya pili mfululizo.
Kwa rekodi hizo, Van Gaal amekiri kufanya makosa
kwa kumwaachia mshambuliaji huyo kuondoka kwenye kikosi chake.
Mdachi huyo aliwaacha pia Robin van Persie,
Radamel Falcao, Adnan Januzaj na James Wilson na kuifanya Man United kukosa
makali kabisa kwenye fowadi yake.
Kikosi hicho cha Old Trafford kimefunga mabao 24
tu katika mechi 20 ilizocheza kwenye
Ligi Kuu msimu huu, mabao sita katika mechi saba za hivi karibuni.
Lakini, Van Gaal alisema kwamba hakutaka kuwapo
kwa ushindani wa namba katika kikosi chake na ndiyo maana aliamua kuwapunguza
baadhi ya wachezaji na kuwaacha wengine.
Van Gaal alipoulizwa kama alifanya makosa kwa
kumwaacha Chicharito, alisema: “Pengine unaweza kuona ukweli kwenye hilo,
lakini usingeweza kulifikiria hapo kabla. Unaweza kuwaaacha washambuliaji wote
kwenye timu, lakini matokeo yake kungekuwa na mafowadi wengi. Ikiwa hivyo
hawatakuwa na furaha na watalazimisha kuondoka.
“Kwa mfano wa hadithi ya Hernandez, alitaka
kucheza. Mimi siamini ushindani, naamini kujiamini na kuaminika. Pengine hilo
ni kosa, lakini nimekuwa nikifanya hivyo katika maisha yangu yote ya ukocha.
Napenda kuwaamini wachezaji.”
Post a Comment