0


MADRID, HISPANIA
KOCHA Rafa Benitez anaweza kufukuzwa baada ya miezi saba ya kuifundisha Real Madrid.
Wakurugenzi wa klabu hiyo ya Hispania wamekuwa katika kikao cha kumjadili baada ya Madrid kushindwa kupata ushindi katika mchezo wa Jumapili dhidi ya Valencia.

Rais wa Madrid, Florentino Perez ameitisha kikao cha bodi Jumatatu mchana ambacho kitafuatiwa na mkutano wa waandishi wa habari.
Matarajio ni kwamba Benitez atatimuliwa na mchezaji wa zamani wa timu hiyo, Zinedine Zidane atachukua majukumu yake baada ya kuachana na timu B ya Madrid ‘Castilla’ hadi mwishoni mwa msimu.

Rais Perez anaaminika ni muumini  na shabiki mkubwa wa kocha, Jose Mourinho na kocha huyo wa zamani wa Chelsea anabaki kuwa chaguo la rais huyo pamoja na kwamba timu kwa sasa atapewa Zidane kwa muda.

Benitez ameshindwa kupata ushindi katika mechi kubwa katika msimu huu kwa kupoteza pointi zote mbele ya Villarreal, Sevilla na Barcelona na  kuambulia pointi moja moja dhidi ya Atletico Madrid, Valencia na PSG.
Real Madrid itafanya mazoezi Jumanne katika viwanja vya Valdebebas ambapo maelfu ya  mashabiki watahudhuria kuwashuhudia nyota wa timu hiyo  wakifanya vitu vyao.
Inadaiwa kuwa, Benitez  hajaambiwa au labda  anajiandaa na mazoezi hayo lakini kwa kiasi kikubwa inaaminika Real Madrid sasa itakuwa chini ya Zidane na siyo kocha huyo wa zamani wa Liverpool. 
Baada ya sare ya Jumapili dhidi ya Valencia, Benitez aliwasili  katika chumba cha mkutano Mestalla na kujaribu kujibu maswali moja baada ya lingine kuhusu hatma yake ndani ya timu hiyo.

“Ninataka kuwahakikishia kuwa tutajituma kwa kila mchezo,” alisema.“ Nadhani usiku wa leo tumefanya juhudi kubwa na ninafarijika na wachezaji.”
Alipoulizwa kama sare hiyo inaweza kumpotezea kibarua chake, Benitez alijibu: “ Hilo ni kama tu tunaangalia matokeo. Kiwango kilichooneyeshwa  kinastahili zawadi kuliko kupondwa.
“ Siwezi kuwazuia watu kupata  hisia kuhusu kazi yangu. Lakini nataka kuwahakikishia kuwa timu imefanya kazi kubwa sana leo.”

“Tumeshuhudia timu kubwa ikiwa na wachezaji 10 waliokuwa wamesimama wakihesabiwa mpaka mwisho, ingewaje tulikuwa na nafasi kubwa ya kushinda.” 
Kapteni wa Real Madrid, Sergio Ramos alisema alifikiri  bosi wake alikuwa na karata ya ziada kwa ajili ya mechi za raundi ya pili  lakini imekuwa rekodi kwa Real Madrid dhidi ya timu bora za upinzani ambao umewasaidia  wale wote wanaotaka mabadiliko.
Shinikizo la kutimuliwa limemwandama Benitez kwa wiki kadhaa kutokana na wapinzani wa jadi Atletico Madrid na Barcelona kuwa juu ya Ligi ya La Liga na mashabiki wa Real Madrid wamekuwa wakipiga  kelele za kutaka mabadiliko.
Mashabiki vichwa ngumu, ambao hawataki kusamehe walionyesha hisia zao mbele ya Benitez Jumatano iliyopita kwa mara nyingine kwa kumzomea katika mchezo dhidi ya Real Sociedad.

Hiyo siyo mara ya kwanza kwa Benetez kuzomewa msimu huu, sauti kama hizo zilisikika uwanjani  baada ya kipigo cha nyumbani dhidi ya Barcelona.
Kipindi kifupi cha Benitez, Santiago Bernabeu kimekuwa na ripoti ngumu huku ikiwadiwa kuwa straika wa timu hiyo, Cristiano Ronaldo na  wachezaji wengine wakubwa hawakubaliani na ufundishaji wake.
Bosi huyo wa zamani wa Liverpool alipondwa mapema kwa kufundisha soka la kujihami.

Post a Comment

 
Top