0


                     LIVERPOOL, ENGLAND
TAKATAKA kabisa. Ndiyo, bora waseme wao kuliko wengine. Wachambuzi mahiri wa soka, huku wawili kati yao wakiwa wameichezea Arsenal kwa mafanikio, wameibuka na kuiponda klabu hiyo baada ya kichapo walichochezea kutoka kwa Liverpool.
Thierry Henry na Martin Keown ambao wameichezea Arsenal kwa mafanikio chini ya utawala wa Kocha wa sasa, Arsene Wenger wameungana na beki wa zamani wa Manchester United, Gary Neville kuponda kiwango kilichoonyeshwa na Arsenal.
Wababe hao wa Jiji la London, Jumapili waliendeleza mdororo wao wa miaka ya karibuni baada ya kukubali kichapo cha mabao 4-0 kutoka kwa Liverpool katika Uwanja wa Anfield huku wakionyesha moja kati ya viwango vibovu katika utawala wa Kocha Wenger.
“Nilitaka kuondoka uwanjani. Sifanani na hiyo timu na nilikuwa natazamia hilo. Wakwame. Nilijua hilo lingetokea tu leo, lakini bado unapoona mambo yanakwenda hivyo, unasema hapana, isitokee tena jamani. Hata hivyo, sishangazwi sana,” alisema Henry.
“Namna ambavyo Arsenal wanapoteza mechi ni tatizo. Tunaongelea kuhusu hamu ya timu na kujitolea kupambana. Inaumiza sana na namna wanavyopoteza mechi ni vilevile tu. Kama shabiki unajaribu kujipa moyo, lakini sio kitu kizuri kuona. Nini kingine? Kila unachokiona leo kimekuwa kikitokea kwa miaka 10 iliyopita,” alilalamika Henry.
Naye Keown, ambaye alikuwa beki nguli enzi zake alihoji mbinu za Wenger kuelekea katika pambano hilo huku akishangaa kwanini alimuacha nje mshambuliaji wake aliyemnunua kwa pesa nyingi, Alexandre Lacazette na kumpanga Danny Welbeck.

               Bao la kwanza lilifungwa na Roberto Firmino
 “Najaribu kukumbuka ni lini Arsenal walicheza kiwango kibovu kama hiki. Ni udhalilishaji. Hawa ni wachezaji ambao wanaonekana kama vile hawataki kuwa hapa. Na kocha anaonekana kama vile amepotea njia yake,” alisema Keown.
“Sioni kama Arsene Wenger anafanya maamuzi sahihi. Kwanini alimuacha nje Alexandre Lacazette aliyenunuliwa kwa rekodi ya klabu Pauni 53 milioni katika mechi muhimu kama hii? Ingeleta maana kumchezesha katika uwanja ambao Arsenal haijashinda kwa miaka mitano,” aliongeza Keown.

Maneee!
“Kwanini Hector Bellerin alichezeshwa kama beki wa kushoto wakati Sead Kolasinac, ambaye ni beki wa kushoto asilia alikuwepo? Kolasinac amecheza vizuri katika mwanzo huu wa msimu. Kwanini Gabriel ameuzwa? Beki, ambaye ana nguvu sambamba na Laurent Koscielny. Ina maana Rob Holding ambaye hana uzoefu, ameingia katika kikosi cha kwanza Aprili alirushwa kwa Mbwamwitu.”
Naye Neville, ambaye anajulikana kwa kuichukia Liverpool akiwa mchezaji wa United alidai, wachezaji wa Arsenal hawastahili kuvaa jezi za timu hiyo.


Sanchez akifuatilia mchezo baada ya kutolewa
“Ni kitu kilichosemwa sana kwamba mimi sio shabiki wa Liverpool, lakini timu hii ya Arsenal ilistahili kuchapwa. Walistahili kabisa. Liverpool ni wazi katika kwenda mbele, lakini unawezaje kucheza hivi katika mechi kubwa na wachezaji kama wa Arsenal?” alihoji Neville.

Salaaaah!
“Achana na habari ya kutojituma, achana na habari ya kucheza vibaya, lakini kiukweli wana tabia ya kukosa heshima kwa jezi. Wachezaji watatu hadi wanne wanashindwa kukimbia wala kujali, ni fedhea kwa klabu kubwa. Nilikuja nikiwa nimetulia leo lakini kwa kweli nimekasirika na nina hasira na sijui mashabiki wao wanajisikiaje,” aliongeza Neville.
Wakati huo huo, Henry alirudi tena kuonyesha wasiwasi kama Alexis Sanchez anaweza kubakia tena klabuni hapo baada ya matokeo ya mechi ya Jumapili.

Sturridge akishangilia la nne
“Tunaongea suala la Sanchez na kwamba anabakia, lakini hawezi kutaka kuwa sehemu ya timu hii. Na ndio maana wachezaji hawasaini mikataba mipya, kuna kitu wanakiona hakipo sawa,” aliongeza Henry, ambaye mpaka sasa ndiye mfungaji bora wa muda wote katika kikosi cha Arsenal.

Post a Comment

 
Top