0


                                   BARCELONA, HISPANIA
LIONEL MESSI sasa ameazimia kuihama Barcelona baada ya miamba ya Ligi Kuu England, Manchester City kufanya kikao na wawakilisha wa mchezaji huyo.
Messi ambaye amefunga mabao 508 katika michezo 585 aliyoitumikia Barcelona tangu mwaka 2004, pia ameisaidia timu hiyo kutwaa mataji manane ya La Laliga na manne ya Ligi ya Mabingwa Ulaya huku akijijenga kuwa mmoja kati ya wachezaji wakubwa kwa muda wote klabuni hapo.
Straika huyo mwenye umri wa miaka 30-alionekana kukubali kujifunga kwa muda mrefu Barcelona kwa kukubali mkataba wa miaka minne mwezi uliopita, lakini ripoti zinasema uhamisho wa kushangaza katika majira haya ya  joto unaweza kutokea.
Habari zinasema, mkutano kati ya viongozi wa Manchester City na wawakilishi wa Messi ulifanyika jijini Barcelona wiki iliyopita, na klabu hiyo ya Ligi Kuu England ikaulizia uwezekano wa Muargentina huyo kutua England.
Inadaiwa Messi anazidi kuchanganyikiwa na hali inayoendelea Barcelona- kufuatia mchezaji mwenzake na rafiki yake Nemar kuuzwa Paris Saint-Germain (PSG) mwezi uliopita pamoja na viongozi wa Barcelona kusisitiza kwa asilimia ‘200’ angebaki.

Barcelona inahangaika kutaka kumsajili mbadala wa Neymar, kutoka Liverpool, Philippe Coutinho ambaye klabu yake imesema hauzwi. Tayari Barca imepeleka ofa tatu na zote zimekataliwa.
Pia, Messi anazidi kuchanganyikiwa na matokeo ya uwanjani baada ya timu yake kupata vipigo viwili mfulululizo kutoka kwa mahasimu wao, Real Madrid katika mchezo wa Hispania Super Cup.
Mchezo wa kwanza ilifungwa mabao 3-1 katika uwanja wa nyumbani wa Camp Nou na ule wa ugenini uliofanyika Bernabeu ilifungwa 2-0.
Man City imeonyeshwa kuvutiwa na Messi kwa miaka kadhaa sasa na Kocha Pep Guardiola ana matumaini ya kumsajili fowadi mwingine kabla ya dirisha la usajili kufungwa Agosti 31.
Straika wa Arsenal, Alexis Sanchez amekuwa akihusishwa kwa kiasi kikubwa kutua Etihad lakini Arsenal na kocha wake, Arsene Wenger hawana mipango ya kumuuza raia huyo wa Chile katika msimu huu wa majira ya joto.

Post a Comment

 
Top