0


LONDON, ENGLAND
KITENDO cha Manchester City kumteua kocha wa zamani wa Barcelona, Pep Guardiola kinamkutanisha kocha huyo na staa wake wa zamani, Yaya Toure ambaye inasemekana walitofautiana wakati akiwa Barcelona na akamruhusu kuondoka klabuni hapo kwenda City mwaka 2010.

 Hii si mara ya kwanza kwa kitendo kama hicho kutokea.
Wayne Rooney vs David Moyes Wawili hawa walikuwa na historia hii. Rooney aliibukia katika mikono ya Moyes wakati wakiwa Everton. Baadaye Rooney akapakaza katika kitabu chake kwamba Moyes alikuwa amelazimisha auzwe kwenda Manchester United kwa dau la Pauni 27 milioni mwaka 2004.
Moyes akamshtaki Rooney na akashinda kesi ya kupakaziwa na Rooney mnamo mwaka 2007. Rooney alilazimishwa kumuomba msamaha Moyes na pia kumlipa fidia ya Pauni 150,000.
Wakati Sir Alex Ferguson alipoachia ukocha Old Trafford, Moyes alipewa kibarua hicho na kujikuta akikutana tena na ‘Mbaya’ wake, Rooney.
Hata hivyo, waliua bifu lao na kuthibitisha kwamba limekufa Moyes alimteua Rooney kuwa nahodha wake.


Jose Mourinho vs Cesc Fabregas 
Kuna kocha mwenye historia ya kukorofishana na wachezaji wa timu pinzani zaidi ya Mourinho? Bifu kubwa la Mourinho na Fabregas lilitokana na upinzani mkubwa uliokuwa unaendelea kati ya Barcelona na Real Madrid wakati huo, Cesc akiwa mchezaji wa Barcelona huku Mourinho akiwa kocha wa Madrid. Fabregas alikuwa anaongoza vijembe kwa Mourinho wakati bifu likiwa limepamba moto.



Wakati Carlo Ancelotti alipotua Real Madrid mara baada ya Mourinho kuondoka Fabregas alisika akisema: “Kwa sasa hatutakuwa na kocha ambaye anakasirika pindi mchezaji wa Real Madrid anapoongea na Barcelona.
” Fabregas alimpiga kijembe Mourinho ambaye alikuwa akikasirika wakati wachezaji wa Madrid walipokuwa wanaongea na wale wa Barcelona.
Miezi michache baadaye Fabregas alikuwa akisaini kuichezea Chelsea kwa dau la Pauni 27 milioni huku akidai kuwa sababu kubwa ya kusaini Chelsea ni kwamba Mourinho alikuwa bonge la kocha.
 Kevin Keegan vs Michael Owen
 Wawili hawa waliwahi kukutana katika kikosi cha timu ya taifa ya England.
Owen alidai kwamba Keegan alikuwa anamuonea kwa kumfanya kisingizio pindi timu hiyo ilipokuwa inafanya vibaya. “Nadhani nilikuwa naonewa. Kulikuwa na presha kubwa kwake na alikuwa anahitaji mtu wa kumtoa kafara. Nilianza kutompenda. Sio kama mtu tu bali kama kocha,” alisema Owen mwaka 2005.
Owen hakufikiria kama siku moja angecheza tena chini ya Keegan hata hivyo, ilitokea tena wakati alipokwenda Newcastle United Januari 2008.
Na siku ambapo Keegan alifukuzwa, Owen alikaririwa akidai kwamba alikuwa na huzuni sana.
“Kilikuwa kipindi bora cha maisha yangu ya soka Newcastle. Kila mtu alipenda kucheza chini yake. Ilikuwa ni fahari kucheza chini yake. Nilifurahia kipindi cha maisha yangu ya soka pale kuliko kipindi chochote nikiwa na Newcastle,” alikaririwa Owen Juni 2013.
Jose Mourinho vs Samuel Eto'o
Kila mtu anakumbuka jinsi staa huyu wa Cameroon alivyotangaza wazi kwamba asingeweza kuichezea Chelsea kamwe. Ilikuwa mwaka 2005 wakati timu yake ya zamani Barcelona ilipopambana na Chelsea katika mechi ya Ligi ya Mabingwa wa Ulaya ambapo Mourinho alianzisha vurugu nyingi uwanjani kiasi kwamba mwamuzi wa pambano hilo, Anders Frisk wa Sweden baadaye aliamua kustaafu soka.
“Kamwe siwezi kusaini timu inayofundishwa na Mourinho. Aliharibu mambo kabisa katika mechi mbili baina yetu.
“Nasisitiza, kocha wa Barca, Frank Rijkaard ni kocha bora licha ya mataji ambayo Mourinho ameshinda,” alisema Eto’o Machi 2005.
Miaka minne baadaye Eto’o alikula matapishi yake wakati alipokwenda Inter Milan kisha Mourinho akahamia klabuni hapo. Baada ya kutwaa taji la Ulaya pamoja alijikuta akisema “Kabla sijaja Inter Milan, hatukujuana vizuri, kwa hiyo uhusiano wetu ulikuwa wa ovyo. “Niliwahi hata kusema kuwa nisingeweza kuchezea timu ambayo Mourinho anafundisha. Lakini Mungu ndiye ajuaye. Alitaka kunionyesha kuwa nilikosea kusema hivyo na leo Jose ni rafiki yangu,” alisema Eto’o, Septemba 2013.

Yossi Benayoun vs Rafa Benitez 
Moja kati ya sababu ni kwa nini Yossi Benayoun aliamua kwenda Chelsea ilitokana na kumkimbia Rafa Benitez akiwa Liverpool. Hakujua kama siku moja Chelsea ingemteua Benitez kuwa kocha wa muda.
Wakati anahama alisikika akisema “Kila mtu ananiuliza sababu za kuondoka Liverpool. kuna sababu moja tu, Rafa Benitez. Kama ningecheza vizuri asingenisifia. Nilipofunga mabao nilitegemea kuwa katika kikosi ambacho kingeanza wiki ijayo.
“Hauwezi kumtendea mchezaji hivyo na utegemee awe na furaha. Benitez alijaribu kuniua kama alivyofanya kwa Riera. Chelsea ilitoa ofa na dili lilishakamilika kabla Benitez hajaondoka,” alisema Benayouna Julai 2010.
Baada ya Benitez kutua na kumkuta Benayoun Chelsea alijaribu kusahau maneno ya staa huyo na kumuingiza katika kikosi chake cha kwanza huku akisema “Benayoun ni sehemu ya timu na anafanya mazoezi na timu. Yossi anaweza kucheza pembeni na najua akili yake ya soka. Hapana shaka anaweza kutupa kitu.”
Cristiano Ronaldo vs Jose Mourinho 

Kuna bifu baina ya Wareno hawa wawili na halikuanzia Hispania.
Lilianzia England wakati Mourinho akiwa kocha wa Chelsea na Ronaldo akiwa staa wa Manchester United.
 Mourinho alimshutumu Ronaldo kuwa alikuwa hana elimu, hajapevuka kiakili, na mengineyo ya kashfa. Ilikuwa ni baada ya pambano lao ambalo Mourinho aliishutumu Manchester United kuwa ilikuwa inapewa penalti nyingi zisizo sahihi huku Ronaldo akijibu mapigo kuwa Mourinho alikuwa ni mgumu kukiri kushindwa kwake.
Miaka kadhaa baadaye walikutana Santiago Bernabeu kama mchezaji na kocha wake na uhusiano wao haukuwa mzuri huku Ronaldo akilalamika kwamba klabu hiyo ilikuwa inakabiliwa na ‘hali mbaya ya hewa’.

El Hadji Diouf vs Neil Warnock 
Ilikuwa ni katika pambano la FA kati ya QPR na Blackburn Rovers Januari 2011 huku Diouf akiwa mchezaji wa Blackburn na Warnock akiwa kocha wa QPR. Diouf alimshambulia kwa matusi mchezaji wake, Jamie Mackie ambaye alikuwa amelala chini ya majeraha akiamini kuwa alikuwa anadanganya.
Ni kweli Mackie alikuwa ameumia na kitendo hicho cha Diouf kiliwakera wengi uwanjani hasa Warnock ambaye mwisho wa mechi alisema: “Nadhani (Diouf) ni mtu asiye na hadhi kabisa. Natumaini aende nje ya nchi kwa sababu sitammiss kumtazama wakati akicheza. Ni mtu mjinga kabisa,” alisema Warnock, Januari 2011.
Septemba 2012, Warnock aligeuka kuwa mnafiki wa hali ya juu kabisa baada ya kuamua kumnunua mshambuliaji huyo wakati akiwa kocha wa Leeds Unted.
Alijitetea akisema :“Hakuna aliyewahi kumsema vibaya zaidi yangu, lakini nilikutana naye katika kipindi cha majira ya joto, baada ya kumwambia ukweli wangu tulimalizana,” alisema Warnock Septemba 2012.

Post a Comment

 
Top