0


                                NA ABEID POLO
HUU ni msimu wa pili. Pep Guardiola akiwa na Manchester City na Jose Mourinho akiwa na Manchester United. Huo ni mlingano wa kwanza baina ya makocha hao wawili wenye upinzani mkali kwenye kazi yao. Kwa msimu huu, kila mmoja ameiongoza timu yake kwenye mechi sita, tano kwenye Ligi Kuu England na moja kwenye Ligi ya Mabingwa Ulaya. Kila mmoja ameshinda mechi tano kati ya hizo na kutoka sare moja. Mlingano mwingine huu baina ya makocha hao. Achana na hilo. Kitu kinachonivutia ni kile kilichoibuka katika Ligi Kuu England. Wameufanya msimu huu kuwa wa timu za kutoka Manchester. Manchester City na Manchester United ndizo timu zinazokabana kileleni, pointi tatu zaidi ya mabingwa hawa watetezi, Chelsea kutoka London.
 Lakini, kwa hii kasi iliyoanza nayo Manchester City na Manchester United, inafanya kuwapo kwa dalili za wazi kabisa  mbio za ubingwa wa msimu huu kwenye ligi hiyo, inaweza kuwa ya farasi wawili. Manchester United na Manchester City au Mourinho na Guardiola. Kila mmoja amecheza mechi tano, amekusanya pointi 13. Kila mmoja amefunga mabao 16 na amefungwa mabao mawili. Wanalingana kila kitu. Kila mmoja alijaribu kutengeneza timu yake kupambana kwenye ligi kuhakikisha kuna kitu kinavunwa katika msimu huu.
Walau kwa Mourinho, msimu uliopita aliokoteza mataji matatu; Ngao ya Jamii, Kombe la Ligi na Europa League. Lakini, kwa Guardiola upande wake, ulikuwa mtupu. Hakukuwa na taji lolote na hiyo ilikuwa mara yake ya kwanza kumaliza msimu mikono mitupu. Haikuwa hivyo tangu huko alikotokea, Barcelona na Bayern Munich.

Msimu huu anapambana na hali yake yasitokee ya msimu uliopita. Wiki hii wawili hao walihamishia vita yao kwenye Kombe la Ligi. Manchester City ilicheza na West Brom ugenini na Manchester United ikiwa nyumbani ilicheza na Burton Albion. Hadithi imeendelea kuwa ileile, kila mmoja amepata ushindi wa mabao.
Manchester United imeshinda mabao 4-1 na Manchester City imeshinda 2-1.
Kwa kasi ya kufunga zaidi ya mabao 19 au 20 katika mechi sita za Ligi Kuu si jambo dogo. Hiki ndicho walichofanya makocha hao wawili katika vikosi vyao. Jose ana mabao 19 na Pep ana mabao 20. Kila mmoja amejipanga vyema na silaha zake. Hiki ndicho kitu kinachofanya ligi ya msimu huu kuwa na mvuto. Ni wazi kabisa, Arsene Wenger, Antonio Conte, Mauricio Pochettino na Jurgen Klopp watakuwa wanakuna vichwa juu ya wapinzani wao wawili. Klopp amekumbana na mmoja wao, Pep na amekutana na alichokutana nacho. Sasa ni dhahiri, wengine waliobaki watakuwa na wasiwasi mkubwa watakapokutana na mmoja wa makocha hao wawili.

Ni suala la kufikirisha pia, wawili hao watakapokutana kwa mara ya kwanza msimu huu. Nini kitatokea. Lakini, kubwa ni kasi hii walioanza nayo, Jose na Pep, wametupa kitu cha kufuatilia kwa karibu!...

Post a Comment

 
Top