0


                     LONDON, ENGLAND
MAMBO yanazidi kupamba moto. Bifu la Chelsea na staa wake, Diego Costa linataka kwenda mbali zaidi kwa sasa. Inaaminika Chelsea inafikiria kumshtaki Costa mahakamani na kumdai kiasi cha Pauni 50 milioni kama ataendelea kugoma kurudi klabuni.
Chelsea inaamini staa huyo wa kimataifa wa Hispania, mzaliwa wa Brazil anavunja masharti ya mkataba wake na klabu hiyo ambayo inamlipa mshahara wa Pauni 185,000 kwa wiki huku mkataba huo ukiwa umebakiza miaka miwili.
Costa ametajwa katika kikosi cha wachezaji 25 wa Chelsea ambao, watashiriki katika Ligi Kuu ya msimu huu, lakini jina lake halipo katika orodha ya wachezaji watakaoiwakilisha klabu hiyo katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya. Inadaiwa kuwa mwenyewe kwa sasa anazungumza na wanasheria wake.
Uhusiano wa Costa na Kocha wa Chelsea, Antonio Conte umekuwa mchungu zaidi baada ya staa huyo kushindwa kufanikiwa azma yake ya kurudi katika klabu yake ya zamani, Atletico Madrid siku moja baada ya kufungwa kwa dirisha la uhamisho la Hispania.
Chelsea imesisitiza Costa bado anaendelea kuwa mchezaji wake na ni lazima arudi kuendelea kuutumikia mkataba wake. Costa anadai uhusiano wake na Chelsea ulikufa pale tu Kocha Conte alipomtumia meseji kwamba, hakuwa katika mipango yake tena.

Costa amekubali kufanya mazungumzo na Chelsea.
Kwa miezi miwili sasa Costa amejichimbia katika Jiji la Rio de Janeiro, Brazil huku akiendeleza vita ya maneno na Conte, lakini sasa suala lao linaweza kwenda pabaya zaidi wakati huu Chelsea ikifikiria kumshitaki.
Chelsea inajulikana kwa masuala ya mahakamani na mara ya mwisho ililazimika kumlipa daktari wa timu yao, Eva Carneiro kiasi cha Pauni 5 milioni baada ya kubwatukiana na kocha wa Chelsea wa wakati huo, Jose Mourinho.
Hata hivyo, inadaiwa kuwa Costa amekubali kukaa meza moja na Chelsea na kufanya mazungumzo ya Amani.
Wakati huo huo, klabu ya Atletico Madrid imemuomba Costa arudi katika mazoezi ya kikosi cha Chelsea kwa ajili ya kumaliza suala hilo na hivyo itamchukua kwa amani kutoka kwa mabingwa hao wa England.
Atletico ndio klabu pekee ambayo inataka kumchukua Costa kwa sasa baada ya kumuuza kwenda Chelsea kwa dau la Pauni 32 milioni katika dirisha kubwa la majira ya joto mwaka 2014.
Tangu hapo Costa na Atletico wamekuwa katika uhusiano mzuri. Endapo Costa atarudi mazoezini Chelsea kuna uwezekano mkubwa akajikuta akiishia katika kikosi cha wachezaji wa akiba, lakini bado atakuwa akijiweka katika nafasi nzuri kujiunga na Atletico dirisha la Januari.
Chelsea imepitia katika kipindi cha ovyo cha dirisha la uhamisho licha ya kufanikiwa kuwanasa mastaa Alvaro Morata kutoka Real Madrid, Tiemoue Bakayoko kutoka Monaco, Danny Drinkwater kutoka Leicester City, Antonio Rudiger kutoka Roma na Willy Caballero iliyemnasa bure kutoka Manchester City.
Mastaa watatu waligoma kujiunga na timu hiyo katika dirisha hili. Romelu Lukaku, Alex Oxlade-Chamberlain, na Ross Barkley wote waliitosa Chelsea na sasa presha imepelekwa kwa wakurugenzi wawili wa Chelsea, Marina Granovskaia na Michael Emenalo.

             Costa akiwa na hasimu wake, Conte enzi zao.
Conte, ambaye amekuwa hana mamlaka ya kisheria katika mazungumzo na wachezaji wapya klabuni, ameonekana kukerewa na suala la wachezaji hao kukataa kuhamia Chelsea huku tajiri wa timu Abramovich akitaka maelezo ya kina kutaka kujua kwanini mastaa hao waliitosa Chelsea.

Post a Comment

 
Top